Msanii Chikuzee amefunguka kuhusu video iliyosambaa mtandaoni mapema wiki hii akiwa anaombewa kanisani baada ya watu kuhoji kuwa huenda amebadili dini kisiri.
Kwenye mahojiano na podcast ya Captain nyota Chikuzee amesema alikuwa ameenda kanisani kwa ajili ya kuomba dua ya kumuondolea mapepo huku akikiri hadharani kuwa kuna baadhi ya wasanii wa Mombasa walimfanyia vitendo kishirikini kumkwamisha kimuziki.
Hitmaker huyo wa “Si Vibaya Kujuana” amekanusha kutumia jina la Mungu kutafutia kiki huku akisisitiza kuwa masuala ya dini sio ya kufanya mzaha.
Hata hivyo amekazia kuwa madai ya kubadilisha dini kutoka uislamu kwenda ukristo hayana ukweli wowote ambapo amewataka walimwengu kuheshimu uhuru wa watu wengine kusalia kanisani au msikitini badala ya kuwapangia nini cha kufanya katika maishani.