Mwanamitandao na msanii Diana Marua amekumbana na ukosoaji mkubwa kutoka kwa mashabiki wake kwa kuvalia vazi la kampuni ya Balenciaga kipindi hiki ambacho kampuni hiyo inakabiliwa na kashfa nzito ya tangazo lenye utata.
Katika video aliyopakia kwenye mitandao ya kijamii, Diana Marua alionekana jikoni akiangalia chajio siku ya Jamhuri ambayo mfanyikazi wake wa nyumba alikuwa akiandaa.
Mashabiki wake hata hivyo waligundua amevalia T-shati yenye michoro ua kampuni ya Balenciaga jambo ambalo liliwafanya watumiaji wengi wa mitandao ya kijamii kushangaa kwa nini mwanamama huyo alivaa bidhaa ya kampuni hiyo wakati huu inaendelea kupata ukosoaji mkubwa duniani.
Watu mashuhuri na mashabiki kote ulimwenguni wametangaza hadharani kuachana na Balenciaga kutokana na kampeni ya aibu ambayo imepelekea watu wengi kupakia video kwenye mitandao ya kijamii, wakichoma bidhaa za Balenciaga
Ikumbukwe Balenciaga inakabiliwa na kashfa ya kufanya photoshoot ya bidhaa zao mpya ambayo inadaiwa kuendekeza maudhui ya ponografia kwa watoto.