Msanii mkongwe kwenye muziki Nyota Ndogo amejipata akiwa kwenye huzuni mkubwa katika kipindi hiki cha sikukuu baada ya watu waliokuwa wamekodisha vyumba vya kulala katika hoteli yake kushindwa kulipia gharama ya huduma aliyowapa.
Kupitia ukurasa wake wa Instagram Hitmaker huyo wa “Watu na Viatu” amesikitishwa na kitendo cha watu hao wanane kudanganya mhudumu wa vyumba hivyo kuwa walimtumia pesa kwa laini yake binafsi kabla ya kutoroka na kuzima simu zao.
Mwanamuziki huyo mwenye makaazi yake Pwani ya Kenya hajaweka wazi ni muda gani watu hao waliishi kwenye vyumba hivyo ila amesisitiza kuwa watakuwa wa mwisho kumfanya vitendo vya kitapeli.
Hata hivyo watumiaji wengi wa mitandao ya kijamii wameonekana kumhurumia kwa utapeli aliofanyiwa huku wakimtaka kuripoti kisa hicho kwa polisi lakini pia wakamshauri kuanzisha mfumo wa watu kulipia kwanza huduma kabla ya kuwapa vyumba vya kulala.