Staa wa muziki kutoka nchini Nigeria Tems ametangaza kuwa hatoweza kutumbuiza kwenye Tamasha la Tukutane Festival kutokana na sababu zilizo nje ya uwezo wake.
Tems amelithibitisha hilo kupitia ukurasa wake wa Twitter na kutoa ahadi kwa Wakenya kuwa siku za mbeleni atatua nchini kwa ajili ya kutoa burudani.
“Kusema kweli, inasikitisha sana kusema haya lakini sitaweza kutumbuiza kwenye Tamasha la Tukutane kutokana na mazingira yaliyo nje ya uwezo wangu.”
“Nimekatishwa tamaa kama ninyi nyote lakini ninatazamia kuja na kuwapa onyesho ambalo mnastahili. Nawapenda nyote.” Ameandika Twitter.
Hata hivyo maelezo hayo ya Tems yanapishana na yale yaliyotolewa na waandaji wa tamasha la “Tukutane” (SIC) ambao wao kupitia taarifa yao waliyoitoa wameeleza kwamba, nyota huyo alishalipwa gharama zake zote siku 15 zilizopita, na tamasha lilikuwa lifanyike Oktoba 15.
Lakini ghafla meneja wa Tems akawaambia Tems hatoweza kuja kwenye onesho hilo, hajisikii kuja Kenya. Waandaaji wa “Tukutane”, (SIC) wameeleza walishtushwa na taarifa hiyo iliyowavunja moyo. Aidha, wameomba radhi kwa mashabiki kufuatia kadhia hiyo na wanatazamia kupanga tarehe nyingine mpya kwa ajili ya tamasha hilo.