Kamati inayojishughulisha na uchaguzi katika Chama cha Wanamuziki nchini Uganda imeridhia ombi la msanii King Saha kuahirisha uchaguzi wa chama hicho ambao ungefanyika Mei 23 mwaka huu.
Kupitia barua iliyochapishwa kwenye mitandao ya kijamii ya chama cha UMA, uchaguzi wa chama hicho umeahirishwa kwa wiki mbili zaidi kutoa nafasi kwa tume ya uchaguzi kuboresha mifumo ya kupigia kura.
Lakini pia kutoa elimu kwa wagombea wa wadhfa wa urais katika chama cha UMA kuhusu mbinu ambayo itatumika kuandaa uchaguzi wa chama hicho.
Hata hivyo duru zimesema kwamba uchaguzi wa UMA umeahirishwa kutokana na shinikizo kutoka kwa umma baada ya watu kutilia shaka mchakato wa upigaji kura kwa njia ya sms ambao ungefanya uchaguzi huo kutokuwa wa haki na huru.
Utakumbuka King Saha anachuana na mwimbaji mwenzake Cindy Sanyu kuwania urais wa Chama cha Wanamuziki wa Uganda.