Rapa Victor Kamenyo amefunguka kwa mara ya kwanza kuhusu sakata la kumdhalilisha kijinsia mchumba wake Angora Akoragye ambapo wengi walihoji kuwa alikuwa anatengeneza mazingira ya kutangaza onesho lake lijalo.
Kwenye mahojiano yake hivi karibuni rapa huyo kutoka Uganda amesema anamheshimu sana mpenzi wake na kamwe hatokuja kumtumia kwenye masuala ya kiki kwani wamekuwa kwenye hatua za mwisho kukamilisha mchakato wa kuhalalisha mahusiano yao.
“Ni mtu ninayempenda sana. Nataka arudi kwa sababu tulikuwa na mipango mingi pamoja. Tulikuwa tunapanga kwanjula mwezi wa Disemba. Mipango ilikuwa tayari,” alisema Kamenyo.
Katika hatua nyingine amekanusha madai ya kumsaliti kimapenzi mchumba wake licha ya jumbe kusambaa mtandaoni zikionyesha alikuwa akiwanyemelea wanawake wengine.
Mapema wiki iliyopita Victor Kamenyo alizua gumzo mtandaoni mara baada ya video kusambaa ikimuonesha akimshushia kichapo cha mbwa mwanamke mmoja anayedaiwa kuwa ni mpenzi wake.
Video hiyo ambayo inadaiwa kurekodiwa na jirani yake imeibua hisia mseto miongoni mwa watumiaji wa mitandao ya kijamii, wengi wakimtaka mwanamuziki huyo achukuliwe hatua kali za kisheria kwa hatua ya kumdhalilisha kijinsia mwanamke huyo.