Msanii nyota nchini Willy Paul ametoa changamoto kwa wasanii wenzake kuzichukulia hatua kali za kisheria kampuni au mapromota wanaokataa au kuchelesha malipo yao wanapotumbuiza kwenye shoo zao.
Kupitia instastory yake kwenye mtandao wa Instagram Willy Paul amesema wasanii waache suala la kuwahurumia wateja wao wanapochelesha pesa zao kwani ndiyo njia pekee watapewa heshima kwenye shughuli zao za kimuziki.
Hitmaker huyo wa “Toto” amesema wasanii wanapodai haki yao mara nyingi makampuni au mapromota huwa wanaingiwa na jeuri kiasi cha kutochukua simu zao kitendo ambacho amedai sio cha kingwana.
Hata hivyo hajabainika ni kitu gani kilichopelekea Willy Paul kutoa madai hayo ingawa walimwengu kwenye mitandao ya kijamii wamehoji huenda kuna mtu amekataa kumlipa msanii huyo pesa zake na ndio maana ameamua kutumia mitandao ya kijamii kutoa ya moyoni kuhusu mapromota au makampuni kuchelesha malipo ya wasanii.