Mwimbani wa Bongofleva toka WCB Wasafi, Zuchu amechaguliwa kutumbuiza kwenye tuzo za AFRIMMA zitakazotolewa Novemba 19 huko Dallas, Texas nchini Marekani.
Kupitia ukurasa wao rasmi wa Instagram, AFRIMMA walipakia video ya kudensi ya Zuchu akicheza wimbo wake mpya wa Kwikwi na kusema kwamba ni rasmi msanii huyo atakuwa miongoni mwa watumbuizaji watakaopamba sherehe hizo. Wameandika;
“Zuchu atatumbuiza moja kwa moja kwenye onyesho la TUZO ZA AFRIMMA mwaka huu. Zuchu ni mwimbaji na mtunzi wa nyimbo kutoka Tanzania mzaliwa wa Zanzibar lakini mwenye makazi yake jijini Dar es Salaam”
Hatua hiyo inakuja siku chache baada ya Zuchu kutajwa kuwania tuzo za MTV EMA katika kipengele cha Best African Act.
Utakumbuka pia Zuchu anawania AFRIMMA katika kipengele cha Msanii Bora wa Kike Afrika Mashariki, anachuana na Nandy, Maua Sama na wengineo.